Jumatano, 11 Machi 2015

WASICHANA WANAOISHI HOSTELI WATAKIWA KUACHA KUPIGIANA ‘STORY’


Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Dk. Rehema Nchimbi


Na Michael Katona, Njombe

WANAFUNZI wa shule za Sekondari nchini wametakiwa kuwa na utulivu wakati wakiwa Hosteli ili kupata muda mzuri wa kusoma na kuacha mara moja kupigiana ‘story’ ambazo zitawafanya wasiwezeshwe na wasijiwezeshe.

“Wanafunzi wasichana mmejengewa hosteli ili muwe na utulivu, muwe na muda mzuri wa kusoma, lakini sina uhakika sana hizo hosteli ‘story’ mnazopigiana ni  za namna gani, Matron inabidi uwe unapita unasikiliza vile vi ‘story’ vyao, hivi ni ‘story’ za Jiography, Mathematics, Physics , Biology za Kiswahili, ni ‘story’ gani?” alisema Dk. Rehema Nchimbi mkuu wa Mkoa wa Njombe.

Akihutubia wananchi wakati wa kilele cha sherehe za Siku ya Wanawake Duniani ambazo Kimkoa zilifanyika katika Kijiji cha Lole, Kata ya Ikuna, Wilaya ya Njombe Vijijini, Dk. Nchimbi alisema mbali ya kuwawezesha wasichana hao, bila shaka muda mwingi wanautumia kwa mambo ambayo yanafanya wasijiwezeshe.

“Mnaweza mkawawezesha hawa wasichana, lakini muda mwingi wanautumia kwa mambo ambayo yanafanya wasijiwezeshe na wasiwezeshwe, tumieni vizuri sana muda wenu nyinyi wasichana mnapokuwa shuleni, jamii imewajengea hosteli, wazazi wanachangia ili muweze kuishi vizuri, tulieni na kila dakika muone mnathamani kubwa kwa ajili ya kuwezeshwa,” alisema Dk. Nchimbi.

Alisema haiwezekani mwanafunzi anayeishi katika hosteli kwa miaka minne halafu anafeli jambo ambalo alisema linamshangaza.

“Haiwezekani kwa miaka mine unakuwa hosteli halafu unafeli, kwa nini ufeli, na huko hosteli? Ukiwa nje ya hosteli unalalamika, unasema unajua nikienda nyumbani ninachota maji mara na kwenda wapi, wavulana na pita wananifinyia macho, sasa nani anakufinyia macho hosteli?,” aliuliza Dk. Nchimbi.

“Kwa nini husomi vizuri wakati ukiwa hosteli, harafu badala ya kufinyiwa macho, wewe mwenyewe ndiyo unafinyafinya macho, daftari,vitabu huoni vizuri, halafu unaanza kusingizia wengine, tunaposema uwezeshaji wa wanawake tuna maanisha kwamba ni haki kuwezeshwa, lakini wanawake sisi tunawajibu kuhakikisha kwamba tunaheshimu, tunathamini, tunatambua na tunatendea haki kwa uaminifu na uadilifu fursa mbalimbali, ” alisema.

Katika hatua nyingine, Dk. Nchimbi aliendesha harambee ya kuchangia ujenzi wa madarasa kwa ajili ya shule ya msingi Lole iliyojengwa tangu mwaka 1976 ambayo iko katika hali mbaya ya uchakavu wa madarasa kwa kukusanya jumla ya shilingi 1,320,000, ambapo ahadi zikiwa ni shilingi 830,000 huku fedha taslimu ni sh. 490,000. Pia jumla ya miche ya miti 500 ilipatikana katika harambee hiyo huku bati 50 kwa ajili ya kuezekea darasa zikiahidiwa kutolewa na Shirika la EADD.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni