Utalii Wetu

ALICHOSEMA WAZIRI MKUU WAKATI AKIFUNGUA KONGAMANO LA UWEKEZAJI NYANDA ZA JUU KUSINI


Wakuu wa Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini wametakiwa kudumisha amani na usalama ili kuvutia uwekezaji endelevu kwa lengo la kukuza uchumi na kipato cha mtu mmojammoja.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mizengo Pinda alipokuwa akifungua Kongamano la uwekezaji Nyanda za Juu Kusini linalofanyika jijini Mbeya.

Pinda amesema kuwa hakuna uwekezaji endelevu na wenye tija katika maeneo yenye fujo, vurugu na uvunjifu wa amani. Amesema kuwa uwekezaji wenye tija mara zote hufanyika katika maeneo yenye utulivu mkubwa na amani.

 Ameutaka uongozi wa mikoa hiyo kutoa nafasi kubwa ya ushirikiano baina ya sekta binafsi na sekta ya umma kutokana na umuhimu wao katika kuleta maendeleo.  

Akiongelea umuhimu wa kongamano hilo, Waziri Mkuu  amesema kuwa lengo la kongamano hilo ni kuibua fikra mpya za mikoa na kanda kujiamini kuwa wanauwezo wa kuvuta fursa za uwekezaji na kukuza uchumi, kuongeza pato la taifa na kupambana na umasikini kwa wananchi.

Amesema kuwa wawekezaji wameanza kuona Dar es Salaam si mahali pekee pa kuwekeza tatizo wanalokumbana nalo hawajapata taarifa za maeneo yenye fursa za uwekezaji.

Pinda ameitaka kanda hiyo kujipanga vizuri katika kilimo cha mbogamboga na matunda kwa lengo la kuinua pato la mikoa hiyo.

Akiongelea kilimo cha mahindi, Waziri Mkuu amesema kuwa nchi ya Tanzania ni ya tano katika Afrika kwa uzalishaji wa mahindi huku ikishika nafasi ya 15 duniani.

Hata hivyo amsema Tanzania ni nchi ya mwisho katika makundi yote mawili katika tija na kuitaka mikoa hiyo kuongeza tija katika kilimo cha mahindi na usindikaji wake.

Akiongelea sekta ya mifugo katika ukanda huu, Waziri Mkuu amesema kuwa wakati kanda hiyo ikijivunia wingi wa mifugo ikiwa na  ng’ombe zaidi ya 1,000,000 na mbuzi zaidi ya 500,000 inakabiliwa na changamoto ya viwanda vya usindikaji nyama.

 Aidha, amemuagiza Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu- Dkt. Mary Nagu kuhakikisha kiwanda cha kusindika nyama cha Mbeya kinaanza kazi mara moja kwa kuwataka wadau wote kukaa pamoja na kutoka na suluhisho.

Waziri Mkuu amewahakikishia wawekezaji umeme wa uhakika. Amesema kuwa serikali imejipanga kuwa na umeme wa kutosha nchini ifikapo mwaka 2015.

Amezitaka mamlaka za serikali za mitaa kuondoa umangimeza na vikwazo visivyo vya lazima katika kuhamasisha uwekezaji. “Msiwe kikwazo, kuweni wawezeshaji. Ninyi si watawala ni waleta maendeleo katika jamii” alisisitiza Waziri Mkuu.

Kongamano la uwekezaji kwa mikoa ya Iringa, Njombe na Mbeya ni muitikio wa agizo la Waziri Mkuu, Mizengo Panda kuhakikisha makongamano yanafanyika katika ngazi ya kanda ili kuweza kuvutia wawekezaji nchini kwa lengo la kukuza uchumi nchini.


NYUMBANITU: Hazina muhimu Nyanda  za Juu Kusini




Kuku wanaopatikana kwenye msitu wa Nyumbanitu ulioko mkoani Njombe



Na Mwandishi Wetu, Njombe

Tanzania ni nchi iliyojariwa neema kubwa ya maliasili, hususan wanyama, hifadhi, milima, misitu na hata vitu vyenye kuvutia kihistoria.

Katika kudhihirisha hilo, tembelea sehemu mbalimbali katika nchi hii ya Tanzania utaweza kujionea na kufurahishwa na namna uumbaji wa Mungu ulivyokuwa wa ajabu.

Kutokana na hilo, Tanzania imekuwa na vitu mbalimbali vya kihistoria baada ya watawala wa kikoloni waliopita kuacha mambo ya kihistoria.

Hayo yanawezekana kuvuta hisia kwa sasa wakati ukianza kusimuliwa juu ya historia na maajabu yaliyopo ndani ya mkoa wa Njombe hasa ukifanikiwa kufika katika maeneo ya kihistoria yenye maajabu yake ambayo yanashawishi kila mmoja kutaka kutembea na kujionea mwenye kile kinachosemwa kuwa kilikuwepo au la!

Kwa mujibu wa mtaalam wa mambo ya kale, ambaye yupo kwenye msitu wa Nyumbanitu, Msigwa yeye anaeleza namna Njombe ilivyojaliwa kuwa na mambo mengi yenye historia ya kipee hapa Tanzania.

Katika simulizi yake, Msigwa anaeleza kuwa hapo kale, msitu wa Nyumbanitu ambao hadi sasa unatumiwa na wananchi wa kabila la Wabena, ambalo ndilo chimbuko halisi la wakazi wa mkoa wa Njombe kwa kuenda ndani ya msitu huo kufanya matambiko ya kimira kutokana na imani zao.
Lakini maajabu makubwa ndani yam situ huo ndiyo yamekuwa yakiwafanya wageni na wananchi wasio wazawa kutaka kujua nini hasa siri yam situ huo kuwa na mambo mengi yenye maajabu yake.

Akisimulia namna ambavyo msitu wa Nyumbanitu ulivyo na maajabu hayo, Msigwa, alisema, katika miaka ya nyuma, raia wa Uingereza kadhaa waliowahi kufika mjini Njombe walikuwa na utaratibu wa kutafuta maeneo kadhaa kwa ajili ya kuwekeza katika kilimo na ufugaji.

Katika shughuli hizo, waingereza hao waliamua kuufyeka msitu huo kwa ajili ya kutayarisha mashamba kwa kilimo, lakini ajabu kubwa ilikuja kujitokeza pale walipoamua kuifyeka miti iliyopo ndani ya msitu huo, jambo ambalo liliwashinda baada ya kujitahidi kuikata miti hiyo lakini haikukatika.

Baadaye maamuzi ya Waingereza hao ilikuwa ni kuichoma moto miti iliyokuwepo ndani yam situ huo, hata hivyo baada ya kuichoma, walijikuta wakazi wa eneo hilo wakitaabika kwa kukosa mvua ya kunyesha eneo hilo kwa muda mrefu, jambo ambalo liliwaladhimu wazee wakimila kuwataka Waingereza hao kulipa Nguo nyeusi, Kuku weusi na Ng’ombe weusi ili hali iweze kurudi kama mwanzo.

Kufuatia kukubali kufanya hivyo kama ambavyo wazee hao wa kimila wamewataka, Waingereza hao walipigwa na butwaa baada ya kuona mvua kubwa ikinyesha wakati huohuo, jambalo ambalo lilielezwa lililotokana na matambiko yaliyofanywa yakuomba mizimu iliyopo ndani ya msitu huo kupitia mzee mmoja aliyefahamika kwa jina la Kyalula.

Kutokana na kadhia ya namna hiyo iliyowahi kutokea ndani yam situ huo miaka hiyo ya nyuma, utamaduni uliokuwepo hivi sasa ndani ya eneo hilo la msitu ni kwamba, hakuna mtu yeyote anayeruhusiwa kukata miti wala kuchoma moto au kuendelea na shughuli yoyote ndani yam situ huo.
Katika simulizi yake hiyo, Msigwa alieleza kwa watu wanaofika ndani ya msitu huo kwa ajili ya mambo mbalimbali ya kimila, utakutana na kuku weusi wawili, ambao ni Jogoo na kuku jike (mtetea), ambao mara nyingi huwa wapo sehemu ya njia ya kuingilia ndani ya msitu huo.
Ajabu kubwa iliyopo wakati unapoingia kwenye msitu huo ni pale njia ya kupitia inaonekana ikiwa ni fupi, kwa kuzungukwa na miti iliyopishana, lakini mtu anayeingia hapo anaelekezwa ajitahidi kuinama mgongo na hairuhisiwi kuruka madhara makubwa yanaweza kukupata.

Vilevile ukiwa kwenye msitu huo, hurusiwi kutembea umevaa viatu, ni lazima uvue viatu vyako, na kwamba kwa mgeni yeyote anayeingia humo hatakiwi kukaidi maelekezo yeyote anayopewa, na iwapo ukiwa mkaidi ukaamua kufanya vile ambavyo unafahamu wewe, unaweza ukajikuta unapata matatizo makubwa, na hata endapo utaamua kurudi ulikotoka huwezi kuona njia ya kutokea.

Ukiwa ndani ya msitu huo, humo utaweza kujionea, mti mmoja ambao umezungushiwa kitambaa cheusi, huku pembeni kukiwa na kigoda, mikuki na nyungo ndogo ambao unatumika kuwekea pesa ambazo zinaelezwa kwamba ni za sadaka kwa ajili ya tambiko na hata wageni wanaoingia humo inatakiwa itolewe.
Ukiondoa vitu hivyo vilivyomo ndani yam situ huo, pia kuna mapango ya ajabu na yenye kustaajabisha yaliyopo umbali wa kilomita 20 katika kijiji cha Mlevela kilichopo jirani na msitu huo wa Nyumbanitu.

Ndani ya mapango hayo, kuna vyumba 45, ambapo katika historia yake imeelezwa na Msigwa kuwa kulikuwa na Ng’ombe waliokuwa wakionekana wakitoka kwenda kuchunga bila ya mchungaji. Na vilevile Ng’ombe hao wakati mwingine walileta taharuki kwa wakazi hao, pale walipoonekana hali ya hewa ilikuwa ikibadilika kwa kuonekana kutanda Ukungu mwingi katika sehemu hiyo.

Katika mapango hayo, sehemu ya vyumba hivyo, vilitumika kwa ajili ya makazi ya Ng’ombe hao, huku sehemu nyingine ndani ya vyumba hivyo ilionekana kuwa ina sehemu ya chumba cha sebule na vyumba vya kulala. Imeelezwa wakati wa vita wakoloni walitumia maeneo hayo kama sehemu ya kujihifadhi, na vilevile ilikuwa ni njia iliyotumika kupitia chini kwa chini na kuja kutokea sehemu ya maporomoko ya maji yaliyopo njia panda ya barabara ya kueleke Makete kutoka Njombe mjini.

Hata hivyo ndani ya mapango hayo, kuna viti vya mawe vilivyopo ambavyo vimegawanyika, kimoja ni cha baba na kingine ni cha watoto, ambacho hadi sasa kwa wageni wanaoingia humo huelekezwa kuwa kiti cha baba hakirusiwi kukaliwa na mtu yeyote kutokana na kupewa heshima ya baba!

Ndani ya mapango hayo, kuna chumba kimoja kilichopo humo kinaonyesha hakiwezi kuwa na mwanga wa aina yoyote, hata kama utawasha tochi au moto, hali ya giza totoro bado ipo palepale. Ukiwa ndani ya chumba hicho kuna maji yakitiririka, ambayo yanaelezwa kuwa yana Baraka kwa mtu atakayeyatumia kwa kunywa na hawezi kupata madhara
 yoyote.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni