Jumatatu, 4 Agosti 2014

Happy Birthday Ice FM Radio 99.3!

Na Mwandishi Wetu, Makambako

Ni kelele za shangwe zilizokuwa zikisikika usiku wa Jumamosi Agosti 2, 2014 baada ya wasikilizaji, mashabiki na wapenzi mbalimbali wa redio Ice FM iliyopo katika Halmashauri ya Mji Makambako wakati ilipokuwa ikifanya sherehe ya kutimiza mwaka mmoja tangu ilipoanza kurusha matangazo yake rasmi.




“Tupo hapa kusherehekea mafanikio makubwa yaliyofanywa na Ice FM redio, ni wachache wanaweza kuanzisha redio na hatimaye kusimama kwa muda mrefu kama hii redio mbayo inatimiza mwaka mmoja leo tangu ilipoanza kurusha matangazo yake mjini Makambako,” alisema Regina Mwanyika mkazi wa Makambako.

Ice FM radio inarusha matangazo yake kupitia masafa ya 99.3 kutoka mjini Makambako, mwishoni mwa wiki ilifanya sherehe kubwa katika uwanja wa mpira wa miguu wa Amani Makambako na kujipongeza, huku ikiwatambulisha rasmi watangazaji wake ambao wamekuwa ndiyo chachu ya kufanya redio hiyo isimame hapo ilipofika hivi sasa.

“Sikiliza ndugu mwandishi, nawapongeza sana hawa jamaa wa hii redio, hasa Mkurugenzi wake McDonald na timu nzima ya watangazaji, wako makini sana, wanaweza kuwa namba moja hivi sasa hapa Mkoani Njombe, kutokana na redio yao hii kuwa na matangazo bora sana, ” alisema Ally Mwakyusa.

Katika sherehe hiyo, burudani mbalimbali zilikuwepo uwanjani ikiwa ni pamoja na kundi maarufu mkoani Njombe la Makhirikiri kutoka wilayani Makete.

Mbali ya kundi hilo, pia msaanii maarufu Sam wa Ukweli kutoka jijini Dar es Salaam naye alitoa burudani yake na hivyo kunogesha sherehe hiyo kabambe iliyovuta maelfu ya mashabiki uwanjani hapo.

Hakika katika sherehe, hakukosi burudani za kila aina, kwani mbali na burudani za muziki, vilevile kulikuwa na mchezo wa kukimbiza kuku, mpira wa soka na mchezo wa ngumi.

Katika mchezo wa soka, timu ya Ice Fm na Uhamiaji zilichuana vikali katika uwanja wa Amani na matokeo yalikuwa 2-0 baada ya Ice Fm kukubali kichapo kutoka Uhamiaji.


Wakati kwenye mchezo wa ngumi, Mkurugenzi wa Ice Fm Radio, Mc Donald alipigana na DJ Jose ambaye ni mtangazaji wa redio hiyo, lakini katika mchezo huo wa raundi tatu, matokeo yalikuwa sare baada ya kila mmoja kuangushwa chini mara mbili.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni