Jumatano, 11 Machi 2015

RC DK. NCHIMBI ATAKA NJOMBE IONGOZE KUUZA MAZIWA, UFUGAJI NCHINI


MKUU wa Mkoa wa Njombe, Dk. Rehema Nchimbi akizungumza na Daina Mangula ambaye ni mshindi wa ufugaji bora Afrika Mashariki na kwa nchi 133 barani Afrika juu ya ufugaji bora wa Ng’ombe wa Maziwa. Kushoto ni Mkurugenzi wa Shirika la Mradi wa Uendelezaji Sekta ya Maziwa Afrika ya Mashariki (EADD) Mark Tsoxo.



Mkurugenzi wa Shirika la Mradi wa Uendelezaji Sekta ya Maziwa Afrika ya Mashariki (EADD) Mark Tsoxo akizungumza na Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Dk. Rehema Nchimbi wakati alipotembelea na kukagua banda la maonyesho la EADD.



Na Michael Katona, Njombe

MKUU wa mkoa wa Njombe, Dk. Rehema Nchimbi amewataka wanawake mkoani Njombe kuchangamkia fursa zinazotolewa sasa na mashirika ya misaada ya kimataifa katika suala la ufugaji wa Ng’ombe wa Maziwa, ambao utasaidia kupata kipato na kuboresha maisha yao kwa ujumla.

“Katika suala la uwezeshaji wanawake, Shirika la Mradi wa Uendelezaji Sekta ya Maziwa Afrika ya Mashariki (EADD), Mkurugenzi, Afisa Mifugo, Afisa Biashara ninataka ndani ya mwaka huu mmoja muwe mmetuwezesha kuonyesha kila dalili ya Njombe kuuza maziwa na kutawala soko la maziwa hapa Tanzania,” alisema Dk. Nchimbi.

Akizungumza katika kilele cha siku ya wanawake Duniani, sherehe hizo Kimkoa zilifanyika katika Kijiji cha Lole, Kata ya Ikuna, Tarafa ya Makambako wilaya ya Njombe Vijijini, aliupongeza mradi wa EADD awamu ya pili unaondelea hivi sasa wa kopa Ng’ombe lipa Ng’ombe katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini ya Njombe, Iringa na Mbeya utaweza kuboresha maisha bora endelevu kwa watu milioni moja katika nchi za Uganda, Kenya na Tanzania ifikapo mwaka 2018.


Mkurugenzi wa Shirika la Mradi wa Uendelezaji Sekta ya Maziwa Afrika ya Mashariki (EADD) Mark Tsoxo akiwa na wafanyakazi wenzake wakati wakizungumza na wananchi wa Kijiji cha Lole, Kata ya Ikuna mkoani Njombe.




Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Sarah Dumba akipata maelezo kutoka kwa wafanyakazi wa Shirika la Mradi wa Uendelezaji Sekta ya Maziwa Afrika ya Mashariki (EADD) alipotembelea banda la maonyesho kwa ajili ya kutoa darasa la ufugaji bora wa Ng’ombe wa maziwa.

“Msingi mkubwa wa ufugaji ni wanawake, kwa hiyo ndugu zangu wa EADD, Serikali ipo tayari kushirikiana nanyi, lakini lazima tushirikiane kwa malengo, ninachotaka nikuona mkoa wa Njombe unaachwa kusemwa semwa sasa kwa mambo ambayo si yake, Njombe ni nzuri, hali ya hewa ni nzuri, ardhi na mazingira yake ni mazuri,” alisema Dk. Nchimbi.

“Nataka iwe Njombe ambayo inasafirisha Maziwa nchi nzima, na Tanzania nzima ibadilike na kunywa maziwa ya Njombe, msingi mkubwa wa ufugaji ni wanawake na katika mnyororo huo wa thamani kuna wakina mama ambao nataka maafisa Kilimo, Biashara, Ufugaji tuwasaidie kulima na kuzalisha malisho,” alisema.

Mkuu huyo wa mkoa wa Njombe aliitaka EADD kwa kushirikiana na maafisa hao kuyatumia kuwa kauli mbiu yao tekelezeki ambayo inatekelezwa sasa.

“Katika kauli mbiu ya siku ya wanawake inasema “Wezesha wanawake, tekeleza wakati ni sasa” hivyo mwaka huu mwishoni tutakutana tukae tufanye tathimini kuona tumefikia wapi katika kufanikisha hilo, wakulima wakubwa wa malisho wawe ni wanawake, wafugaji wakubwa wazuri na waaminifu wawe wanawake,” alisema Dk. Nchimbi.

Alimpongeza mwanamke  Daina Mangula ambaye alikuwa mshindi wa ufugaji bora katika nchi 133 akitoka kijiji cha Ibumila, Kata ya Kichiwa mkoani Njombe, kwa kuwa mfano mzuri wakuigwa na wanawake wengine katika suala la kujifunza ufugaji wa Ng’ombe wa Maziwa.

“Wanawake ni waaminifu sana katika shughuli zozote zile na hasa zinazohusiana na chakula na afya, wanawake hawawezi kuuza maziwa ambayo wameambiwa wakati wake wa kuuza haujafika, lakini wengine kwa tamaa ya fedha wanakamua kabla ya siku,” alisema.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mradi wa EADD,  Mark Tsoxo aliishukuru serikali kwa kushirikiana nao kuboresha maisha ya wafugaji wanawake kwenye mikoa ya Njombe, Iringa na Mbeya na katika kutekeleza hilo, EADD imekubali kumsaidia mwanamke Wema Kingimbwiti mkazi wa Ikuna ambaye mlemavu na mwimbaji wa kwaya, mtaji wa shilingi milioni moja katika eneo la ufugaji.

“Tutakwenda na wataalamu wetu anakoishi kufanya tathimini na kuona kipi ambacho anakiweza, sisi tutamtayarishia mpango wa biashara, tutahakikisha anapata mtaji usiopungua thamani ya shilingi milioni moja,” alisema Tsoxo.

Naye Lightness Munisi, Afisa Maendeleo ya Jamii na Jinsia wa Mradi wa EADD, alisema malengo ya mradi ni kusaidia wafugaji 35,000 wa ng’ombe wa maziwa nchini Tanzania, katika maeneo yenye fursa kubwa ya kuongeza uzalishaji.

Akielezea mradi wa EADD ulivyoanza na mafanikio makubwa, Afisa Mawasiliano Rachael Singo alisema ulianzishwa mwaka 2008 kwa ufadhili wa Bill & Millinda Gates Foundition na umeweza kutoa mafunzo ya ufugaji bora kwa nchi za Uganda, Kenya na Rwanda huku kwa upande wa Tanzania mradi huo unategemewa kuongeza wigo na kuunganisha nguvu ya pamoja ya wafugaji na usawa wa kijinsia katika kaya 36,000 nchini.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni