Jumatano, 18 Machi 2015

Israel yaanza uchaguzi mkuu

Vituo vya kupigia vimefunguliwa kote nchini Israel hii leo asubuhi katika uchaguzi mkuu ambao unatarajiwa kuamua hatma ya Waziri mkuu Benjamin Netanyahu ambaye amekuwa madarakani kwa miaka sita.

Zaidi ya wapiga kura milioni tano na laki nane wanatarajiwa kupiga kura kuwachagua wabunge wapya 120 katika uchaguzi ambao unaonekana kama kura ya maoni kuhusu utawala wa Waziri mkuu Benjamin Netanyahu na chama chake cha Likud.

Akizungumza baada ya kupiga kura yake asubuhi katika shule moja mjini Jerusalem, Netanyahu amesema hataunda serikali ya muungano na chama cha leba iwapo atashinda, bali ataunda serikali ya kizalendo na vyama vya mrengo wa kulia.

Netanyahu anatafuta muhula wa nne madarakani lakini itachukua wiki kadhaa ya mazungumzo kuhusu kuundwa kwa serikali ijayo baada ya uchaguzi kujua iwapo atasalia madarakani au atabanduliwa na mpinzani wake wa karibu Isaac Herzog wa chama cha sera za wastani cha umoja wa Uzayuni.

Katika siku ya mwisho ya kampeni hapo jana, Netanyahu aliapa kuwa hataruhusu kuundwa kwa taifa la Palestina iwapo atachaguliwa tena na kuwarai wapiga kura kumchagua ili wapinzani wake wasiingie madarakani na kuhujumu usalama wa Israel na udhibiti wa mji wa Jerusalem.
Waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu akipiga kura

Hii itakuwa mara ya tatu Israel inafanya uchaguzi mkuu tangu mwaka 2009 badaa ya Netanyahu kulivunja bunge na kuitisha uchaguzi wa mapema kufuatia tofauti ndani ya serikali yake ya muungano iliyotishia kuusambaratisha utawala wake.@dw

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni