Jumatatu, 12 Januari 2015

SAKATA LA IPTL: Mabalozi waitaka Serikali kuchukua hatua kali

Balozi wa Vatican nchini, Francisco Montecillo Padilla (kushoto) akizungumza na Balozi wa Saudi Arabia nchini, Hani Mominah wakati wa sherehe za mwaka mpya ziliyoandaliwa kwa ajili ya mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao na mashirika ya kimataifa. Picha na Anthony Siame 
Dar es Salaam. Licha ya Rais Jakaya Kikwete kutoa ufafanuzi wa sakata la uchotaji fedha kutoka Akaunti ya Tegeta Escrow iliyokuwa Benki Kuu na kutangaza kuchukua hatua dhidi ya baadhi ya viongozi na watendaji, nchi wahisani wamesema bado suala hilo linawachanganya na wanasubiri tamko la Serikali.
Nchi hizo, ambazo zilizuia takriban Sh1 trilioni za ufadhili na kuchangia nakisi ya bajeti ya Serikali, juzi zilikiri kuanza kuruhusu sehemu ya fedha hizo baada ya baadhi ya maazimio ya Bunge la Jamhuri ya Muungano kuanza kutekelezwa, ikiwa ni pamoja na kumvua uwaziri Anna Tibaijuka, kumsimamisha kazi Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi na kumuweka kiporo waziri wake, Sospeter Muhongo na kusababisha Jaji Fredrick Werema kujivua wadhifa wake wa Mwanasheria Mkuu.
Tayari Rais Jakaya Kikwete ameshaeleza kuwa fedha hizo hazikuwa za Serikali.
Hata hivyo, akizungumza na gazeti hili juzi, Balozi wa Jumuiya ya Ulaya nchini, Timothy Clarke alisema kwamba Serikali imeonyesha jitihada za mwanzo, lakini wanasubiri kuona hatua kali zaidi zikichukuliwa pamoja na kuja na kauli moja kuhusu fedha hizo.
Alisema alichobaini ni kwamba wananchi wengi wanataka kujua hatima ya sakata hilo ndiyo maana walitumia vyombo vya habari kufanya mijadala mbalimbali kuzungumzia wizi wa fedha za escrow ambazo haijawekwa wazi kuwa ni za umma ama ni za Kampuni ya Kufua Umeme ya IPTL.
Balozi Clarke alisema kwa upande mwingine, Serikali imeonyesha tabia ya kusita katika kutoa uamuzi kwenye suala hilo na kwamba walitarajia kusikia tamko kali pamoja na tamko la kuzuia vitendo hivyo visiendelee.
Alieleza kuwa hadi sasa nchi nyingi hazijaipa fedha Tanzania kama zilivyokuwa zinatarajiwa kwa kuwa bado zinasubiri hatua zaidi kutoka serikalini.
Sakata la escrow, lililohusu uchotwaji wa Sh306 bilioni kutoka akaunti hiyo, lilisababisha Taasisi ya Marekani ya MCC inayosaidia nchi zinazoendelea, kutangaza kusitisha kusaini mkataba wa awamu ya mpango huo wa maendeleo kuishinikiza Serikali kushughulikia kashfa hiyo.
Bodi ya Wakurugenzi ya MCC ilitoa taarifa yake Desemba 16 mwaka jana, ikieleza kuwa mkutano wake wa Desemba 10 mwaka huu uliruhusu kuanza maandalizi ya kusaini mkataba wa awamu ya pili ya mpango huo, lakini ulielezea hofu na masikitiko kuhusu hali ya rushwa inavyoendelea Tanzania.
Fedha ambazo Tanzania ilipaswa kupata kupitia mradi huo wa MCC awamu ya pili ni Dola 450 milioni ambazo ni sawa na Sh765 bilioni.
“Japokuwa bodi ilipiga kura kwa dhati kabisa ya kuiruhusu Tanzania iendelee na maandalizi kwa ajili ya mkataba wa pili, inaihimiza Serikali ya Tanzania kuchukua hatua thabiti na mahsusi za kukabiliana na rushwa kama sharti la msingi kwa bodi hiyo kufanya uamuzi wa mwisho wa kuidhinisha mkataba huo.


Sakata la escrow lilihusisha fedha zilizokuwa zimehifadhiwa Benki Kuu wakati kesi baina ya Shirika la Umeme (Tanesco) na IPTL zikipambana mahakamani. Pande hizo mbili zilikubaliana kufungua akaunti hiyo ya escrow ili kutunza fedha ambazo Tanesco ilitakiwa iilipe IPTL ikiwa ni malipo ya ununuzi umeme.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni