Jumatatu, 1 Desemba 2014

RC NCHIMBI: NAPENDA KUFANYA KAZI MKOA USIO NA MAAMBUKIZI YA VVU


Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Ghalib Bilal akiwa na Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Rehema Nchimbi wakipokea maandamano ya kilele cha Siku ya Ukimwi Kitaifa



Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Ghalib Bilal  akihutubia


Mbunge wa Njombe Kaskazini, Deo Sanga akiwa na mkuu wa mkoa wa Njombe, Dk. Rehema Nchimbi akicheza muziki pamoja na wana kwaya wa KKKT Makambako






Na Michael Katona, Njombe

MKUU wa Mkoa wa Njombe, Dk. Rehema Nchimbi amemweleza Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Ghalib Bilal na wananchi wa mkoa wa Njombe kuwa anapenda kufanya kazi katika mkoa ambao hauna maambukizi ya VVU.

“Hili ndilo tukio langu la kwanza la kitaifa tangu ni hamie kuwa mkuu wa mkoa wa Njombe, wananchi wa Njombe nimefika Njombe, naipenda Njombe, na niko tayari kufanya kazi Njombe, lakini ni Njombe ambayo haitakuwa na Ukimwi,” alisema Nchimbi.

Mkuu huyo wa mkoa alikuwa akitoa salamu zake kwa mgeni rasmi Makamu wa Rais wakati wa maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani, ambapo Kitaifa yalifanyika mkoani hapa kwenye uwanja wa Sabasaba.

“Wakati kiwango cha maambukizi ya VVU kikishuka Kitaifa kutoka asilimia 5.7 mwaka 2007/08 hadi kufikia asilimia 5.1 mkoa wa Njombe mwaka 20011/12 mkoa wa Njombe kiwango cha maambukizi kiliongezeka hadi kufikia asilimia 14.8,” alisema Nchimbi.

“Mh. Makamu wa Rais hali hii haikubaliki na haikubaliki kabisa na hasa kwa Njombe hii ya sasa, mkoa umeandaa mpango wa utekelezaji kwa miaka mitatu ambao ulizinduliwa na Waziri Mkuu mwezi Julai mwaka jana, na mpango huo ulianza kutekelezwa mwezi huo huo mwaka jana,” alisema Dk. Nchimbi.

Mkuu huyo wa mkoa alitaja mpango huo ulipojikita zaidi kuwa ni katika suala la kinga dhidi ya maambukizi ya virusi vya Ukimwi, kupunguza mila na desturi potofu zinazoweza kuchangia kasi ya maambukizi ya Ukimwi, kudhibiti kasi ya maambukizi ya VVU kwa vijana, pia kutoa tiba na msaada kwa wagonjwa wa Ukimwi majumbani na wengine wanaoishi na VVU na utoaji wa dawa za kurefusha maisha kwa wagonjwa wa ukimwi na wale wanaoishi na maambukizi ya VVU,” alisema mkuu huyo wa mkoa.

Aidha Nchimbi alisema katika mkakati huo, kwa mkoa wake wa Njombe umeanza kuonyesha mafanikio makubwa, ambapo idadi ya vituo vya huduma inavyotoa huduma ya tohara kwa wanaume vimeongezeka kutoka vituo 7 hadi kufikia vituo 13 Juni mwaka huu.

Sambamba na hilo, Dk. Nchimbi alisema asilimia ya maambukizi ya mama kwenda kwa mtoto yamepungua kwa kasi kutoka asilimia 12.5 hadi asilimia 9.6 na kueleza kuwa tangu mkoa wa Njombe ulipoanza kuadhimisha maadhimisho hayo kuanzia Novemba 24 na kufikia kilele chake Desemba Mosi, kumekuwa na upimaji wa hiari kwa wananchi, na kwamba lengo lilikuwa ni kupima watu 3,000, lakini  hadi kufikia Novemba 30, mwaka huu jumla ya watu 6,367 waliopimwa kati yao watu 328 walionekana kuwa na virusi vya ukimwi na hiyo ni sawa na asilimia 5.2.

Nchimbi alisema katika takwimu za TACAIDS zimeonyesha wilaya ya Makete ndiyo inayoongoza kwa maambukizi ya VVU ambapo ina asilimia 7.2, na Ludewa ina maambukizi machache ya asilimia 2.5.

“Hakika tukiamua inawezekana na tunaweza kabisa kuwa na Njombe isiyo na maambukizi mapya ya Ukimwi, Njombe isiyo na unyanyapaa na tunaweza kabisa kuwa na Njombe ambayo haina vifo vinavyotokana na Ukimwi,” alisema Nchimbi.

Mkuu huyo wa mkoa wa Njombe alimwomba Makamu wa Rais kuwe na mkakati na dhamira ya kweli ya kufikia mahali kusiwe na siku ya ukimwi Tanzania.


“Inawezekana kabisa kuwa na mfumo wa kitaifa wa kuiondoa Njombe yenye sifa ya muda mrefu yakuwa kinara wa maambukizi ya ukimwi, hii ni Njombe yenye hadhina kubwa sana ya madini ya Chuma, Makaa ya Mawe na inayostawisha mazao mengi, sasa lazima tufike mahali tuwe na Njombe ambayo haina jina la kuwa kinara wa maambukizi ya Ukimwi, hivyo Njombe inatakiwa iwe ni lango kuu lenye rasilimali kwa uchumi wa Tanzania,” alisema Dk. Nchimbi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni