Alhamisi, 9 Oktoba 2014

WALEMAVU WALALAMIKIA UBAGUZI WANAOFANYIWA KWENYE MABENKI

Walemavu wakuongea na kutokusikia (viziwi) wakifurahia kuangalia noti halali ya Tanzania wakati wa Semina ya kutambua noti halali iliyotolewa mjini Njombe jana na Maofisa wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT).

Na Mwandishi Wetu, Njombe

Taasisi za Fedha na Benki mbalimbali nchini zimelaumiwa kuwa zimekuwa zikifanya unyanyasaji kwa walemavu wasiojiweza pindi wanapokwenda kupata huduma za kifedha.

Malalamiko hayo yatolewa juzi mkoani Njombe wakati wa semina iliyokuwa ikiendwa na Benki Kuu Tanzania (BOT) kwa walemavu viziwi na wasioweza kuzungumza kutoka shule ya Viziwi ya mkoani hapa kwa ajili ya kuwapa uelewa wa kuzitambua noti halali na bandia.

Wakizungumza kwenye semina hiyo iliyofanyika katika hoteli ya Miriam, baadhi ya washiriki wa semina hiyo walidai kwamba, wamekuwa hawafurahishwi na tabia ya baadhi ya watoa huduma kwenye benki hizo wakati kwenda kupata huduma za kifedha au kutaka kufungua akaunti kufuatia wafanyakazi wa vitengo hivyo kuwapa majibu yasiyoyakistaarabu.

“Nilipoomba kufungua akaunti katika benki moja hapa mjini Njombe (jina la benki tunalihifadhi) walisema kwa sisi hatuwezi kukufungulia akaunti, kwa sababu wewe ni kiziwi, nililia niliumia kweli,” alidai mshiriki huyo na kukataa kutaja jina lake.

Alisema kufuatia hali hiyo ilimbidi amtufate bosi wake kwa ajili ya kwenda kuzungumza na wafanyakazi wa benki hiyo ili wamsaidie kufungua akaunti hiyo.

“Alipokuja bosi wangu, niliwauliza wafanyakazi hao wa benki, kama asingekuja bosi huyu, je walemavu wengine ambao ni bubu na wasiosikia wangepataje huduma zenu?” alisema mshiriki huyo.

Mlemavu huyo ambaye ni kiziwi aliwataka maofisa hao wa BOT waliokuwa wakitoa mafunzo hayo kuwasiliana na benki na Taasisi za fedha nchini kuondoa kero ambayo wamekuwa wakikutana nayo walemavu mbalimbali hususan vipofu, walemavu wa miguu na wasiosikia ili kupata haki sawa kama raia wengine nchini.

“Naomba mabenki yote ya binafsi au taasisi za serikali waelimishwe kuhusu kuwapokea viziwi, kwa sababu wote ni binadamu au sisi viziwi hatukupenda kuwa hivi,” alisema.

Akizungumzia juu ya malalamiko hayo, Meneja Msaidizi wa kitengo cha Sarafu kutoka BOT, Abdul Dollah alisema anakubaliana na madai hayo kwa kuwa katika sehemu nyingi duniani kuna baadhi ya majengo yanayokuwa na ofisi za kifedha kutokuwa rafiki kwa walemavu.

“Majengo mengi hapa nchini yaliyojengwa wakati huo hayakuwa rafiki kwa walemavu wanaotumia baiskeli za miguu mitatu, hivyo ni vyema hivi sasa mabadiliko yafanyike ili kuweza kuwasaidia wenye tatizo la kufika kupata huduma,” alisema Dollah.

Awali akifungua semina hiyo ya mafunzo kwa viziwi, Meneja Msaidizi kutoka kitengo cha Sarafu BOT Kanda ya Nyanda za Juu Kusini iliyopo Mbeya, Grolia Mwaikambo alisema Mkurugenzi wa Kikundi cha Sanaa na Viziwi Tanzania, Habib Mrope aliomba ufadhili wa kupata pesa kutoka BOT kwa ajili ya kutoa mafunzo kwa viziwi ili yaweze kuwasaidia kutambua noti halali na zile za bandia.

“Lengo letu ni kuisukuma serikali kutoa elimu ya mafunzo kwa hawa walemavu wa viziwi kufahamu na kutambua pesa halali na pesa bandia, ndiyo maana tumeanza kufanya semina hii katika mkoa wa Njombe, lakini pia tunakwenda kwenye mikoa ya Ruvuma na Singida kwa ajili ya kutoa elimu hiyo,” alisema Habib Mrope kwenye semina hiyo.

Naye Vicky Msina ambaye ni Meneja Uhusiano Msaidizi kutoka Idara ya Uhusiano wa Umma (BOT), alisema wameanzisha semina hiyo  kusaidia hasa walemavu wasioona na ambao hawasikii kuweza kugundua utapeli wowote utakaokuwa ukifanywa na watu wenye nia mbaya dhidi ya walemavu hao kwa kuwa wao pia baadhi yao wanafanyabiashara mbalimbali hapa nchini.


“Semina hii itasaidia sana kuweza kuwakamata watu wanaotawanya pesa za bandia, na vilevile itawasaidia walemavu kuwabaini wadanganyifu wanaotumia pesa zisizo halali kwenye maeneo yao ya biashara,” alisema.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni