Alhamisi, 9 Oktoba 2014

POLISI NJOMBE YATAJA WANAFUNZI WANAOSHIKILIWA KWA KUCHOMA BWENI

Wanafunzi wakiwa chini ya ulinzi wa polisi

Na Michael Katona, Njombe
  
KUFUATIA wanafunzi wa shule ya Sekondari Njombe (NJOSS) kufanya vurugu kubwa juzi ikiwemo ya kuchoma moto bweni na kuteketeza jengo hilo, Jeshi la Polisi Mkoani Njombe limetaja majina ya wanafunzi 15 ambao wanashikiriwa kwa ajili ya kufikishwa mahakamani.

Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani hapa, Fulgence Ngonyani jana ametoa taarifa yake na kuwataja majina wanafunzi ambao watapandishwa kizimbani kujibu tuhuma hizo mara upelelezi utakapokamilika.

Ngonyani aliwataja wanafunzi hao wanaosoma kidato cha tano na sita kwenye shule ya Njombe Sekondari kuwa ni Juma Maganga, Seme Charles, Riwad Ngowi, Martin Mhagama, Kenedy Kibangali, Jimmy Mkadenge na Shukuru Kilingo.

Wanafunzi wengine ni Linos Lindu, Kalvin Kisiga, David Swela, Francis Emmanuel, Timothy Minga, Ezra Charles, Johson Mbelele na Ndanga Obadia.

Katika taarifa hiyo ya jeshi la polisi, Kamanda Ngonyani amesema wanafunzi hao walichoma moto karakana ya shule, vifaa mbalimbali vya wanafunzi, walivunja duka la shule ambalo lilikuwa na bidhaa mbalimbali zikiwemo soda na kunywa, kisha wakavunja chupa na kumwaga soda hizo chini.

Pia wanafunzi hao walivamia nyumba mbili za mwalimu mkuu wa shule na mwalimu wa nidhamu na kuvunja vioo vya nyumba hizo sambamba na kuharibu gari namba T809BBX Toyota Carina.

Kamanda Ngonyani alitaja thamani halisi ya mali zote zilizoharibiwa katika vurugu hizo ni Shilingi 113,050,000 Milioni. Alisema kiini cha tukio hilo ni kusimamishwa masomo kwa wanafunzi 29 waliodaiwa kutoroka shuleni hapo mnamo Septemba 6, mwaka huu usiku na kwenda kucheza disko katika ukumbi wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii Njombe kilichopo jirani na shule hiyo.

Alisema wanafunzi hao wakiwa kwenye ukumbi wa disko walifanya vurugu zilizosababishwa na kugombea wanawake, kutokana na vurugu hizo mmoja wa wanafunzi hao alitoka ukumbini na kukimbia ndipo alipoingia kwenye shimo na kuvunjika mguu.

“Wakati anahojiwa na uongozi wa shule ni wapi aliumia mguu alijieleza kuwa alitoroka na wenzake kwenda disko ndipo wakati anarudi akatumbukia kwenye shimo na kuvunjika mguu huo, lakini wanafunzi wengine waliotajwa kwenda disco walikataa,” alisema Ngonyani.
Wanafunzi hao Oktoba 7, mwaka huu walisimamishwa na uongozi wa shule hiyo, lakini siku hiyo majira ya saa 3.00 usiku baadhi ya wanafunzi hao waliosimamishwa masomo na wengine ambao hawajasimamishwa masomo wakaanzishaa vurugu hizo wakipinga maamuzi ya uongozi wa shule hiyo.


Kufuatia vurugu hizo, Afisa Elimu wa mkoa wa Njombe, Said Nyasiro juzi alitangaza kuifunga rasmi shule hiyo hadi Novemba 8, mwaka huu, ambapo wanafunzi wote wametakiwa kurudi na fedha shilingi 150,000 pamoja na barua yakujieleza.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni