Jumatatu, 6 Oktoba 2014

MNYIKA: CHADEMA ITAKWENDA MTAANI KUJADILI RASIMU MBILI ZA KATIBA


Hivi ndivyo ilivyokuwa shwari Makambako, hata Polisi huyu wa kike hakuweza kutumia nguvu nyingi kudhibiti vurugu kwenye mkutano wa Chadema



Naibu Katibu Mkuu Chadema Tanzania Bara, John Mnyika akiwa na viongozi wengine wa Chadema  alipokuwa kwenye mkutano mjini Makambako


John Mnyika akionyesha rasimu ya Jaji Warioba iliyopendekezwa na wananchi 



Naibu Katibu Mkuu Chadema Zanzibar, Salum Mwalimu akizungumza kwenye mkutano mjini Makambako




Makamu Mwenyekiti wa Bavicha Patrick Ole Sosopi akitambulishwa 



Askari wa kike wa Jeshi la Polisi mjini Makambako akisimamia ulinzi kwenye mkutano


Na Mwandishi Wetu, Makambako

Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Maendeleo na Demokrasia (CHADEMA) Tanzania Bara, John Mnyika, amesema hivi sasa watakutana na wananchi mtaani kwa ajili ya kujadili rasimu mbili zilizopendekezwa na Bunge Maalum la Katiba pamoja na ile Katiba ya Jaji Warioba iliyopendekezwa na wananchi.

“Sisi tunasema tukiwa mtaani tutajadili katiba zote mbili, rasimu ya katiba ya wananchi na ile rasimu ya katiba ile katiba haramu, katiba ya mafisadi, sisi wengine tunaunga mkono rasimu ya katiba iliyowasilishwa na Jaji Joseph Warioba inayoungwa mkono na wananchi,” alisema Mnyika.

Akihutubia kwenye mkutano wa hadhara katika Halmashauri ya Mji Makambako, kwenye uwanja wa Jeshi la Polisi mjini hapa Mnyika alisema kuanzia sasa Chadema itakwenda jimbo kwa jimbo eneo kwa eneo kujadili katiba zote mbili. Na kuongeza kuwa Chadema wanataka katiba iliyopendekezwa na wananchi iwe ndiyo katiba ya nchi na kuboreshwa kidogo.

“Warioba alisema hivi na nina kubaliana nao, kwamba wao wanajiita wako wengi kule ndani ya bunge, tutakutana nao mtaani, sasa ndiyo tumekutana nao mtaani, sawa sawa wananchi?” Mnyika aliwauliza wananchi na wanachama wa Chadema waliokuwa wakimsikiliza huku wakimshangilia.

Akihutubia mkutano huo ambao ukiwa na ulinzi wa kutosha kutoka jeshi la polisi, Mnyika alisema kutokana na Bunge la Katiba kuamua kupitisha rasimu ya katiba kwa ajili ya kuipeleka mtaani ili wananchi waijadili, Chadema kuanzia sasa itapita mtaani nchi nzima kuwaeleza wananchi kuipinga katiba hiyo iliyopitishwa na Bunge Maalum.

“Kwa sheria mbovu ya mabadiliko ya katiba, kwa dhamira mbovu iliyokuwa mwanzo kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambayo haikuwa na dhamira ya kuandika katiba mimi naona ni jambo zuri ni jambo la kheri pamoja na gharama zake kwetu wananchi, kwamba tumefikia hapa kuwa na rasimu mbili,” alisema Mnyika.

“Tuna rasimu wanayoiita rasimu iliyopendekezwa, Katiba haramu, tunayo katiba haramu ya Sitta (Samweli), Chenge (Andrew Chenge) na wenzake,  harafu tunayo rasimu ya katiba ya wananchi, ni jambo zuri kwamba sisi Watanzania tunao uwezo wa kuchagua katiba,” alisema Mnyika.

Alisema uamuzi uliofanywa na bunge la Katiba chini ya Mwenyekiti wake Samweli Sitta wa kuipigia kura katiba na kisha kuipitisha kumefanya Tanzania kuingizwa kwenye maajabu ya kupiga kura duniani.

“Tuliwaambia tunahitaji mrekebishe muundo wa bunge lenyewe linaloiandika katiba, kwa sababu sasa hivi bunge limetengenezwa kutafuta kura za CCM, mamlaka makubwa ya Rais yalikuwa ni kuteua wajumbe, nilibishana nao wakaongeza wajumbe 166 mpaka 201 lakini kuna kitu hawakukifanya tulibishana nao sana,” alisema Mnyika.

Aliongeza, “Najua watu wa usalama wanarekodi, Rais Jakaya Kikwete akaonyesha udhaifu mkubwa, akatumia madaraka vibaya katiba lile kundi la 201 akateua makada wa CCM wengi, lengo kuu ni kutafuta theluthi mbili, na theluthi mbili hiyo haikuanza kutafutwa kwa kuchakachua hizi kanuni, kuingiza kifungu ambacho kina iingiza Tanzania kwenye maajabu ya upigaji kura wa dunia nje ya bunge.”

Kufuatia maamuzi yaliyofanywa na bunge la katiba kupitisha rasimu hiyo iliyopendekezwa, Mnyika aliwaambia wananchi kwenye mkutano huo kuwa watanzania hivi sasa wanao uwezo wa kuchagua hizo rasimu mbili.

“Wakati wanafunga Bunge Maalum la Katiba, Pinda (Waziri Mkuu, Mizengo Pinda), Makinda (Spika wa Bunge la Jamhuri, Anna Makinda), Kificho (Spika wa Bunge la Wawakilishi Zanzibar Pandu Ameir Kificho), Sitta (Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba) na kila anayezungumza anasisitiza kwamba, jamani mlio nje mkienda kwa wananchi rasimu ni moja tu, katiba iliyopendekezwa ni moja tu msiwaambie wananchi kuhusu ile katiba nyingine,” alisema Mnyika.

Mnyika pia aliwataka wananchi wakiwa kwenye majimbo yao hivi sasa, kuwaambia wabunge wa Bunge Maalum la Katiba na Wajumbe waliopitisha rasimu hiyo  ya Katiba bungeni kurudisha fedha walizo kula.

“Kuna aina mbili za kuwataka warudishe fedha za wapiga kura, aina ya kwanza ni kwamba, kila ukimuona mbunge wa CCM na Mjumbe wa Bunge Maalum mwambie ‘haramia wewe rudisha fedha zetu’, kwa sababu wamedhamiria kuzunguka nchi nzima kuwaeleza uzuri wa rasimu yao hiyo, sasa wakija kwenye mikutano waambieni…’maharamia nyinyi rudisheni fedha zetu’ tumeelewana wananchi,” alisema Mnyika.

Naibu Katibu Mkuu huyo wa Chadema Tanzania Bara, alisema alipokuwa anahutubia mkutano wa hadhara mkoani Mwanza alisema alitumia neno la uharamia kwa kuwa mwaka 1958 hayati Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere aliwaambia wakoloni wakati anadai uhuru.

“Mwaka 1958 Mwalimu Nyerere alishtakiwa mahakamani na mkoloni, alisema wakuu wa Wilaya ya serikali ya kikoloni ni mashetani na maharamia kwa sababu hawasikilizi malalamiko ya wananchi, kwa hiyo wakamfungulia kesi ya kuwaita mashetani na maharamia na akashtakiwa mahakamani na kajijitetea mahakamani ni kweli nimewaita maharamia na mashetani kwa sababu matendo yao ya kutosikiliza malalamiko ya wananchi ni matendo ya kiharamia na mashetani,” alisema Mnyika akimnukuu Nyerere.

“Sasa Sitta, Chenge na wenzake anasema kwa kuwaita maharamia ni jambo la kitoto, sisi kuwaita maharamia tunafanya siasa za chuoni hatuwezi kuchukua nchi, Mwalimu alipokuwa anafanya mkutano wa TANU alifanya mambo ya kitoto wakati ule, nilisema Nyerere akiwa Mwenyekiti wa TANU alipokuwa anafanya mikutano, bahati nzuri aliweza kuchukua nchi, sasa sisi kwa kuwaita jina lao harisi kwamba ni maharamia tunafanya watu wengi zaidi walioko wajue kwamba hawa ni maharamia ili tufanye kazi ya kuwaondoa kwenye uongozi wa nchi kuwa rahisi zaidi,” alisema Mnyika.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Vijana la Chadema, (BAVICHA), Patrick Ole Sosopi akizungumza kwenye mkutano huo alishangazwa na hatua ya Marais wastaafu wa Tanzania kwa kuwa kimya wakati wa msuguano uliokuwepo wa Chama cha Mapinduzi na Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) juu ya rasimu ya katiba wakati wa Bunge Maalum la Katiba lililopokuwa likiendelea.

“Tuna rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi (Awamu ya Pili), Rais Benjamin Mkapa (Awamu ya Tatu), tunaamini ni watu wenye busara kubwa, tunaamini kama walifikia hatua ya kuliendesha taifa hili, tunaamini ni washauri wazuri wakutuelekeza tuende wapi, nini tufanye kama Taifa, lakini ni watu wamekuwa waajabu sana, tunaandika katiba ya watanzania wote bila kujali itikadi, kuna msuguano mkubwa sana wa Ukawa na CCM, wamenyamaza kimya, hatusikii wakizungumza lolote, leo anaonekana Warioba ndiyo mtu mzalendo kwa wapinzani, lakini Mkapa na Mwinyi wako kimya,” alisema Sosopi.

Wakati huo huo, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Zanzibar, Salum Mwalimu amesema kwamba Katiba iliyopigiwa kura na Bunge Maalum mjini Dodoma na kupelekwa kwa wananchi,  Wazanzibar hawako tayari kuipitisha.

“Zanzibar wakituletea tutaulizana tu, yakhee ya bara hiyo hapo waachieni wenyewe, haituhusu, hatuitaki kwa sababu haibebi maslhai mapana ya Wazanzibar, hata kufunguliwa haitafunguliwa na tumeshawaambia na Zanzibar tumeshapewa mwelekeo, katika taifa lolote duniani, Mwanasheria Mkuu ndiyo msimamizi, mshauri wa masuala ya sheria na katiba katika nchi husika na ndiyo maana mikataba yote ya Tanganyika lazima ipite kwa kwa mwanasheria mkuu, huyo amepewa mamlaka  na katiba, sasa Zanzibar tulishamaliza kazi, kupitia kwa mwanasheria Mh. Othman  Masoud Othman,” alisema Mwalimu.

Alisema Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Othman amepiga kura ya wazi hadharani na kuuonyesha ulimwengu kwamba wanachokiandika, wanachokijadili hakina maslahi kwa Mzanzibar na kwa kura ya wazi akapiga hapana.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni