Jumanne, 7 Oktoba 2014

CWT NJOMBE: BRN INATUZIDISHIA MZIGO WALIMU


Mkuu wa Wilaya, Sarah Dumba akizungumza

Na Mwandishi Wetu, Njombe

CHAMA cha Walimu Tanzania (CWT) Wilayani Njombe kimeitaka serikali kufanya tafiti za kutosha katika miradi yake ukiwemo mradi wa matokeo makubwa sasa BRN ambao wanadai umekuwa ukiwazidishia mzigo wa kuwajibika zaidi bila ya kuongewa kwa ujira.

Pia CWT kimeitaka serikali kusitisha biashara huria ya vitabu vya kiada kutokana na kukinzana kwa baadhi ya vipengele hali inayowasabishia ugumu katika ufundishaji na kuishauri serikali endapo ikishindwa kudhibiti  iwe inahariri vitabu hivyo sambamba  na kuvigonga mihuri ili kuwahakikishia walimu.

Akizungumza katika siku ya walimu iliyofanyika katika Halmashauri ya Mji wa Makambako Mkoani Njombe, Katibu wa chama hicho Wilayani Njombe, Salama Lupenza alisema kuwa kumekuwepo na mafanikio katika mradi wa BRN, lakini wanasikitishwa  na mradi huo kutowaangalia walimu  na badala yake kuwaongezea majukumu bila ya kuwaongezea ujira wowote  wakati ambao  huduma yao kutoka serikalini ikiendelea kusuasua.

Lupenza alisema kufuati hali hiyo, wao walimu wanaona litahatarisha elimu kwa wanafunzi ambao wamekuwa wakiwafundisha nchini.
 

"Tunaona BRN hawakufanya utafiti wa kutosha, kwa sababu kama unashindwa kumwezesha mwezeshaji wa mradi huo usitegemee majibu mazuri na hii inatokana na kuangalia zaidi upande wa mwanafunzi na siyo mwalimu ambaye bado anavilio vingi pamoja na mshahara mdogo, pesa za likizo ni tatizo kwa maana hiyo tunaishauri serikali  iwe inatushirikisha katika mipango yake," alisema Lupenza.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Sarah Dumba ambaye alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho hayo, aliwataka walimu kuendelea kufanya kazi kwa kuzingatia kanuni na taratibu yakiwemo maadili ya mavazi, huku akiwasihi kuacha tabia ya kukopa katika taasisi za fedha ambazo zimekuwa haziweki wazi masharti yao wakati serikali ikiendelea kutatua kero zao.

"Mwalimu ni kioo cha jamii, serikali kwa upande wake itaendelea kutatua kero zenu ikiwemo kero ya mazingira mazuri ya kazi, na nina imani siku moja hizi kelele zote zitaisha kwa jinsi mipango ilivyo hata hiyo miradi ya BRN mnadai kuwa imewekwa kwa ajili ya utekezaji zaidi  imewekwa kwa ajili ya jamii iliweze kupunguza matatizo mbalimbali," alisema Dumba.

Akizungumzia juu ya maadhimisho hayo, Mwalimu Sikujua Joel anayefundisha shule ya msingi alisema kuwa ili kila mtoto aweze kupata elimu  bora na inayostahili nchini ipo haja ya serikali  kutochanganya Siasa na Elimu hasa kwenye mitaala ya  kufundishia, sambamba na kuuchunguza upya mradi wa matokeo makubwa sasa ikiwa ni pamoja na kuufanyia marekebisho ili uweze kuleta tija kwenye  sekta ya elimu.

"BRN hatujaandaliwa kuipokea tumeletewa tu na mabosi zetu, na kwa sasa hatuna hatuna uwezo wa kuizuia, lakini  tunapochukua mradi kutoka nchi nyingine wawe wanaangalia na kufananisha na hali ya kwetu,  siyo kutuletea siasa, hatuwezi kufanya kazi bila ya posho kwa sababu watakaoumia zaidi ni wanafunzi," alisema Mwalimu Joel.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni