Ijumaa, 8 Agosti 2014

Wakulima wa matunda Ludewa wajiandaa na ujio wa wawekezaji


Na Nickson Mahundi, Ludewa

Wakulima wa Matunda wilayani Ludewa katika mkoa wa Njombe wameanza kujipanga na kilimo cha mazao hayo ili kuwauzia wawekezaji wa machimbo ya Chuma cha Liganga na Makaa ya mawe Nkomang’ombe ambao wanatarajia kuwasili wilayani humo hivi karibuni.

Akizungumza na mwandishi wa habari, mmoja wa wakulima hao ambaye anaishi katika kijiji cha Mkongobaki wilayani hapa mzee Edward Mligo (69) alisema kutokana na hali inavyoonesha ya upanuzi wa barabara za maeneo ya migodi inavyoendelea wakulima wengi wamehamasika kujiandaa kwa biashara.

Mligo alisema mpaka sasa yeye binafsi ameweza kupanda miti ya matunda aina ya Machenza na Machungwa ipatayo mia tatu ambayo tayari imeshanza kuzaa matunda na ameshaandaa shamba jingine lenye ukubwa wa hekari 5 kwa ajili ya kupanda miche ya matunda hayo ambayo imeshandaliwa.


Hata hivyo amewataka vijana kuacha tabia ya kukaa vijiweni bila kazi badala yake wajikite katika shughuri za uzalishaji mali ikiwemo kilimo cha matunda na ufugaji ambao utawapa utajiri wa miaka mingi ijayo tofauti na wanavyotarajia.

“Tunaishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuikumbuka wilaya ya Ludewa kwani tumeanza kuona dalili za kufanikisha machimbo ya madini yetu kutokana na barabara zinazoelekea migodini kuanza kupanuliwa tofauti na awali tulikua tukipewa maneno matupu pasipo vitendo”, alisema Mligo.

Hivi karibuni Serikali kupitia wakala wa barabara nchini TANROAD wameweza kutiliana saini na wakandarasi wanne kwa gharama ya kiasi cha shilingi 7.8 bilioni ili kuzipanua barabara za wilaya ya Ludewa na kuweka changalawe kwa ajili ya upitishaji wa mitambo ya migodini.

Ukarabati wa barabara hizo umewaamsha wakulima na wafugaji walioko wilayani Ludewa kujianda na ugeni wa wawekezaji ambapo baadhi ya wakulima wa matunda akiwemo mzee Mligo wamekuwa wakishinda mashambani ili kuhakikisha wanatumia fulsa ya kilimo kujipatia kipato kwa wawekezaji hao.

Aidha wadau mbalimbali wa maendeleo wilayani Ludewa akiwemo Huruma Mgaya wamesifu mpango wa Serikali pamoja na Mbunge wa jimbo la Ludewa Mh. Deo Filikunjombe kwa kazi nzuri ya ujenzi wa barabara za lami katika mitaa ya Ludewa mjini na upanuzi wa barabara kuu kutoka Njombe hadi Ludewa.

Mgaya alisema hali ya upanuzi wa barabara kuu hutaharakisha maendeleo wilayani humo ingawa wananchi walio wengi wanashauku ya kuwa na barabara ya lami itakayounganisha wilaya ya Ludewa na ile ya Njombe kwani msimu wa mvua kiwango hicho cha changalawe huharibika vibaya.

Aliwataka wanaludewa wanaoishi mbali kuchangamkia fulsa za uwekezaji wilayani humo mapema kabla wageni hawajanza kufanya mambo yao.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni