Jumatatu, 4 Agosti 2014

MISS MAUREEN AUZUNGUMZIA UREMBO

  • Ahaidi kusaidia mapambano dhidi ya VVU
  • Mama Maureen: Tusizuie ndoto za watoto wetu
Na Michael Katona, Njombe

“Msichana kushiriki mashindano ya urembo, si uhuni, na sidhani kushiriki urembo ni kukiuka maadili, ni mchezo kama ilivyo michezo mingine,” anasema Maureen Godfrey, akiwa amekaa na mama yake, Maria Itala, wakati alipofanya mahojiano maalum hivi karibuni.

Maureen, akiwa Miss Redds Mkoa wa Njombe, alifanikiwa kutwaa taji la Miss Redds Nyanda za Juu Kusini baada ya kuwashinda warembo wengine kutoka mikoa ya Iringa, Mbeya, Ruvuma, na Rukwa.

Ni jambo la kujivunia katika Mkoa mpya wa Njombe kutokana na ukweli kwamba ni mara ya kwanza kufanya shindano la kumtafuta mrembo wa mkoa. Pia Njombe kama mkoa imeshiriki kwa mara ya kwanza na kufanikiwa kumtoa mshindi wa kuwakilishi kanda ya Nyanda za Juu Kusini katika shindano kuu la kumtafuta Miss Redds Tanzania mwaka 2014.

“Tatizo kubwa ni mtazamo uliopo hivi sasa kwa jamii kuwa warembo wanapovaa pale jukwaani nusu uchi, ndivyo wanachukulia kwamba mashindano hayo ni ya kihuni, lakini si hivyo, ila ni mrembo mwenyewe inategemea amelelewa namna gani na wazazi wake,” anaongeza kusema Maureen.

Mbali na kuwahimiza wazazi wa mkoa wa Njombe kuwaruhusu mabinti zao kupenda kushiriki mashindano hayo ya urembo, Maureen anasema akiwa balozi wa mkoa wa Njombe kwenye mashindano ya kumsaka Redss Miss Tanzania mwaka huu, ataendeleza kampeni ya serikali kuhamasisha jamii kupitia kwa warembo wenzake kupiga vita maambuki ya virusi vya Ukimwi (VVU).

“Hili suala la ugonjwa hatari wa Ukimwi, sitakuwa nyuma katika kulipigia kampeni ili warembo wenzangu pia watambue kwamba ni hatari kwa jamii, nitakapokuwa kambini, nitasimama na kutoa ushauri nasaha, elimu ya namna ya kujikinga na maambukizi,” anasema Maureen.

Akizungumzia changamoto ambazo mkoa wa Njombe imekuwa ikishindwa kutoa warembo kutokana na wazazi wengi kutokuwa na mwamko wa kuwaruhusu mabinti zao wanaotaka kushiriki, mama yake mzazi, Itala aliwaasa wazazi wenzake kuachana na imani potofu kuwa urembo ni uhuni.

“Sioni mantiki ya wazazi wenzangu mkoani Njombe na sehemu nyingine kuwakataza warembo wanaotaka kushiriki mashindano, ni wajibu wao sasa wajue msichana anapoguswa kutaka kushiriki wasimzuie,” anasema Itala.

Mama huyo mzazi wa Maureen alitolea mfano alivyofanya kwa mwanae kwa kuamua kumruhusu kushiriki mashindano hayo na hatimaye kushinda taji la Miss Njombe na kuwakilisha Nyanda za Juu Kusini.

“Mwanangu alikuja na kunieleza mama mimi nataka kujaribu kushiriki Miss Njombe, bila hiyana nilimruhusu ashiriki na nilikwenda kushuhudia mashindano, sikuamini wakati matokeo yanatangazwa kwamba mwanangu ndiye Miss Njombe,” anasema Itala.

“Hata alivyokuwa anafanya mazoezi sikuwa na matarajio yoyote, inashangaza sana na hata tulipokwenda kumpa ‘sapoti’ katika mashindano ya Nyanda za Juu Kusini, nako pia nilijikuta nashangazwa ni bahati gani mwanangu ameipata,” anasema Itala.

Mzazi huyo wa Maureen aliwataka wazazi wasiwe wazito kuwatoa mabinti zao pale wanapohitaji kushiriki mashindano hayo, na kwamba jambo la muhimu ni kuwatia moyo katika mashindano hayo.

“Maureen aliniomba niende kuangalia tukio la Miss Kanda, na akanieleza tukija sisi wazazi na marafiki tutamtia nguvu na kufanya vyema, lakini ni maajabu kweli binti yangu amefanya vyema tena katika shindano hilo,” anasema Itala.

“Kitu cha msingi na rai yangu kwa wazazi wenzangu ni kuona ni jinsi gani ambavyo amempa msingi mtoto wake wa kike kutoka awali, kwani mashindano hayo yanalenga kumpa uelewa endapo atashinda basi yeye ndiyo kioo cha jamii,” aliongeza Itala.

Aidha mama Maureen anasema binti yake tangu ashiriki mashindano hayo anaamini ulikuwa ni ushindani, lakini jambo ambalo anapaswa kuliendeleza kwa binti yake ni kumkanya asipotoke kwenye maadili aliyokuwa ametoka kwa kujitambua, eti hivi sasa yeye ni mrembo maarufu.

“Najaribu kumuasa na kumwangalia mwenendo wake, lakini hii yote ni kumchunga asipotoke, na mweleza wewe ni mtoto wa kike unatakiwa kujiheshimu na kujijali na kujitambua katika jamii, tatizo wazazi wengi hasa sisi Waafrika hatuna tabia ya kumuambia mtoto wa kike wazi ni madhara gani anayoweza kuyapata endapo atajiingiza katika mapenzi akiwa mdogo,” anasema.

Mzazi huyo aliwataka wanawake hususan wazazi wa Njombe kuiga mfano alioufanya yeye, wajitoe kuwaruhusu watoto wa kike kushiriki katika mashindano hayo kwa kuwa yanafaida kwa msichana.

“Mbali na kupata faida yake binafsi, mtoto wangu ameweza kutambulika, lakini pia mashindano hayo yanaleta sifa ya mkoa alikotoka, mfano ameuletea sifa mkoa mpya wa Njombe, lakini pia ameweza kupiga hatua ya kuwa Miss Nyanda za Juu Kusini,” anasema Itala.

Mrembo Maureen ambaye kabila lake ni Mnyakyusa, akizungumzia historia yake ya masomo, anasema elimu ya msingi alianza kuipata kupitia shule ya Arage iliyopo Jijini Mbeya, ambapo baadaye alijiunga na kidato cha kwanza hadi cha nne katika shule ya St. Marys iliyopo pia jijini Mbeya.

Baada ya kuhitimu kidato cha nne, hakuweza kufanya vyema na hivyo wazazi wake walimtaka ajiendeleze kwa kuamua kujiunga na masomo katika Chuo cha Tumaini kilichopo Iringa ambapo alichukua masomo ya Biashara, na hivi sasa ni mwaka wake wa mwisho wa kuhitimu masomo hayo ngazi ya Diploma.

Mrembo Maureen katika mashindano ya Redds Miss Tanzania ataiwakilisha Njombe, wakati mrembo Martha John ambaye ni Miss Iringa 2014 na Naba Magambo Miss Ruvuma 2014, ndiyo watakaowakilisha  Nyanda za Juu Kusini kwenye kinyang’anyiro hicho.

Mtazamo na ushauri: Piga namba 0753-827444

Email:princemichaelkatona@gmail.com

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni