Ijumaa, 8 Mei 2015

Nape amvaa Pinda mgomo wa madereva


Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye  
Dar es Salaam. Wakati Waziri Mkuu Mizengo Pinda ameunda kamati kwa ajili ya kushughulikia mgomo wa madereva uliotikisa nchi kwa siku mbili, katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye amesema haoni mantiki ya kuunda tume kuchunguza jambo ambalo linafahamika.
Wajumbe wanaounda kamati hiyo ni makatibu wakuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Kazi na Ajira na Wizara ya Uchukuzi.
Wengine ni wajumbe watatu kutoka Chama cha Wamiliki wa Malori Tanzania (Tatoa) na wajumbe watatu kutoka Chama cha Wamiliki wa Mabasi (Taboa), mjumbe mmoja kutoka Kikosi cha Usalama Barabarani na mmoja Sumatra.
Pia wanaingia wajumbe wengine watano ambao wanawakilisha madereva baada ya mkuu wa wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda kukubaliana na viongozi wao juzi.
Lakini Nape haoni kama kulikuwa na haja ya kuunda kamati ya kushughulikia tatizo ambalo linajulikana.
“Kama huundwa kuchunguza mambo ambayo hayafahamiki, lakini madai ya madereva hao yanafahamika,” alisema msemaji huyo wa chama tawala alipotakiwa kuzungumzia maoni ya baadhi ya wananchi kwamba mgomo huo ni matokeo ya CCM kushindwa kuwajibika na hivyo kutostahili kuendelea kupewa nafasi ya kuongoza nchi.
“Watupe au watunyime kura, ni kweli CCM na Serikali yake inapaswa kutatua suala hilo. Ndiyo maana mimi nasema sikubaliani na tume. Serikali ishughulikie suala hili kwa kuwa madai ya madereva hao yanafahamika,” alisema Nape.
“Mimi sioni mantiki ya kuunda tume kwa tatizo ambalo linajieleza. Madai ya madereva na wamiliki wa magari yanajulikana, tume ya nini?” alihoji.
Madereva waliendesha mgomo huo nchi nzima wakipinga uamuzi wa serikali kuweka sharti jipya la kwenda kupata mafunzo ya muda mfupi kabla ya kupewa leseni upya na kutaka Serikali iwalazimishe waajiri wao kuwapa mikataba inayozingatia maslahi yao.
Wakati Nape akisema hayo, CCM mkoani Mbeya imeilaumu Serikali kwa kuchelewesha mazungumzo na madereva na hatimaye kusababisha mgomo huo kuwaathiri wananchi bila sababu za msingi.
Katibu mwenezi CCM mkoani hapa, Bashiri Madodi alisema Serikali ilipaswa kuchukua hatua za haraka kutatua tatizo hilo ili kuondoa kero wanazozipata  madereva.
Alisema CCM inawapa pole wananchi walioathirika na mgomo huo na inalaani ucheleweshwaji uliofanywa na Serikali.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni