Jumatano, 18 Machi 2015

Baada ya kufukuzwa, Zitto aigawa mitandao ya kijamii


Mitandao ya kijamii imeanza kuchukua nafasi na hata kuwa sehemu ya maisha ya kawaida, watumiaji wake hupata taarifa mbalimbali na pia nafasi ya kuanzisha mijadala motomoto.
Hata hivyo, changamoto kubwa iliyopo katika mitandao hiyo ni ugumu wa kudhibiti mijadala, hivyo wakati mwingine taarifa nyingine zinakosa ukweli na kuhitaji vyanzo zaidi ili kuzithibitisha.
Suala la Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe kushindwa kesi na hatimaye kuvuliwa uanachama na chama chake cha Chadema, limekuwa sehemu ya mjadala na malumbano makali katika mitandao ya kijamii.
Ili taarifa iaminiwe na wasomaji, mitandao mingi ilinukuu akaunti ya ‘twitter’ ya Kituo cha redio cha East Africa kilichoitoa taarifa ya Zitto kama habari mpasuko.
Katika taarifa hiyo, alinukuliwa Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu akitangaza rasmi Zitto kuvuliwa uanachama.
Katika baadhi ya mitandao majibizano kati ya watetezi wa Zitto na upande wa pili, yalionyesha kama makundi hayo yangekuwa ukumbini kuna tukio baya lingeweza kutokea kwa upande mmoja kushindwa kujizuia na kuanzisha mapigano.
Hii inatokana na ukweli kwamba mbunge huyo ana mashabiki wengi kwenye mitandao ya kijamii na pengine ni miongoni mwa wanasiasa wachache wanaojitokeza hadharani kwenye mitandao na kushiriki mijadala bila woga.
Kama kuna suala linalohitaji ufafanuzi kutoka kwa Zitto, mashabiki wake hawalazimiki kusubiri kauli yake kwenye magazeti kesho yake kwa kuwa hachelewi kutoa maelezo kupitia kwenye akaunti zake kwenye mitandao.
Hata baada ya uamuzi wa Mahakama Kuu iliyotupilia mbali pingamizi lake la kutaka asijadiliwe na chama chake, baada ya muda mfupi Zitto aliibuka katika mitandao ya kijamii akitoa ufafanuzi wa kilichotokea.
“Hatukuwa na wito wa Mahakama leo. Jaji kahamishiwa Tabora. Hatuna taarifa ya Jaji mpya. Mwanasheria wetu anafuatilia na atatoa maelezo,’’ alisema kupitia mtandao wa Twitter.
Uandishi wake kwa kiwango kikubwa ulikidhi mahitaji ya watumiaji wa mitandao ya kijamii ambao wengi hupenda kusoma sentensi fupi fupi na zinazoeleweka kuliko maelezo marefu yenye ajenda tofauti.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni